Connect with us

Ni rasmi kuwa mataifa yatakayoshiriki katika fainali ya mataifa bingwa barani Afrika kuanzia mwaka 2019, yataongezeka na kufikia 24 kutoka 16.

 Kamati Kuu ya Shirikisho la soka barani Afrika, imeidhinisha mabadiliko haya mapya baada ya kongamano la siku mbili kumalizika mjini Rabat nchini Morocco.

Hata hivyo, imekubaliwa kuwa michuano hii itaendelea kuandaliwa kila baada ya miaka miwili barani Afrika.

Mabadiliko mengine ni kuwa fainali hii sasa itachezwa mwezi Juni na Julai na sio mwezi Januari na Februari kama ambavyo imekuwa ikishuhudiwa.

Hatua hii ilifikiwa baada ya kuwepo kwa malalamishi kuwa wachezaji wengi wanaocheza soka barani Ulaya huwa wanapata wakati mgumu kurudi kuzichezea timu zao na hata vlabu vyao kuwazuia kufanya hivyo kwa sababu ya michuano katika ligi wanazocheza.

Mbali na michuano hii ya AFCON, imekubaliwa kuwa mfumo wa michuano ya klabu bingwa na Shirikisho utasalia kama ulivyo. Vlabu vitaendelea kumenyana katika hatua ya mwondoano katika hatua ya makundi na kufuzu katika hatua ya robo fainali, nusu fainali na fainali. Mechi zitaendelea kuchezwa nyumbani na ugenini.

Pamoja na hilo, michuano hii sasa itachezwa mwezi Agosti na kumalizika mwezi Mei na sio kumalizika Novemba kama ambavyo imekuwa ikishuhudiwa.

Aidha, CAF imesema inawekeza katika utafiti wa Kisayansi kubaini chanzo cha wachezaji wengi kuzirai na kupoteza maisha wanapokuwa uwanjani na kuimarisha hali zao za kiafya.

Imekubaliwa pia kutakuwa na michuano ya kikanda ya kufuzu katika fainali ya vijana wasiozidi miaka 17, 20 na 23 kufuzu katika fainali ya bara Afrika.

Kuhusu michuano ya CHAN kwa wachezaji anaocheza soka nyumbani iliyopangwa kufanyika mwaka ujao nchini Kenya, maafisa wa CAF watakwenda kufanya uthathmini wa mwisho mwezi Agosti kabla ya kufikia uamuzi wa mwisho.

Kumekuwa na wasiwasi kuwa huenda Kenya ikapoteza nafasi hiyo kwa sababu ya ukarabati na ujenzi wa viwanja vipya, unaokwenda taratibu.

Wakati wa mkutano huo CAF, ilibainika kuwa Zambia ilijiondoa kuwa mwenyeji wa michuano ya vijana wasiozodi miaka 23 mwaka 2019.

Klabu ya Sudan ya Hilal El Obeid nayo iliruhusiwa kucheza katika hatua ya robo fainali ya michuano ya Shirikisho baada ya Shirikisho la soka duniani FIFA, kuondoa kifungo ilichokuwa iweiwekea nchi hiyo.

More in