Connect with us

Shirikisho la soka nchini Kenya FKF, limekerwa na kusikitishwa na hatua ya Shirikisho la soka barani Afrika CAF, kubadilisha uamuzi wa awali wa timu ya taifa ya soka ya wanawake, Harambee Starlets kushiriki katika mashindano ya bara Afrika inayoanza tarehe 17 mwezi huu nchini Ghana.

Kenya ilikuwa imeruhusiwa kushiriki katika mashindano hayo, baada ya kuondolewa kwa Equitorial Guinea iliyopatikana na kosa la kumchezesha mchezaji wa taifa la Cameroon katika kikosi chake.

Hata hivyo, Equitorial Guinea imekuwa ikisisitiza kuwa mchezaji huyo Annette Jacky Messomo, ni raia wa nchi hiyo na kukata rufaa, ambayo ilizaa matunda na CAF kukubaliana nayo.

Uamuzi huo wa CAF, unamaanisha kuwa, Equitorial Guinea imerejeshwa katika mashindano hayo na inachukua nafasi ya Kenya ambayo ilikuwa imejumuishwa katika kundi moja na Nigeria, Afrika Kusini na Zambia.

Rais wa FKF Nick Mwendwa, ameiandikia barua na kutaka kuahirisha mashindano hayo au yaendelee lakini yaruhusiwe kuwa na mataifa tisa yatakakayoshiriki.

Aidha, Mwendwa anasema, FKF haikufahamishwa kuwa Equitorial Guinea imekata rufaa baada ya uamuzi wa awali wa kuwaondoa katika mashindano hayo.

Habari hizi mbaya, kwa Harambee Starlets zilikuja, wakati ikicheza mechi ya kirafiki na BlackQueens ya Ghana na kumalizika kwa bao 1-1.

 

More in AWCON