Connect with us

 

Kocha wa klabu ya soka ya Gor Mahia nchini Kenya Mbrazil Jose Marcelo Ferreira, amejiuzulu.

Marcelo anayefahamika kwa jina maarufu kama Ze Maria, amemwandikia barua Mwenyekiti wa klabu hiyo Ambrose Rachier siku ya Alhamisi na kumwambia kuwa anaachana na klabu hiyo.

Kocha huyu na mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Brazil mwenye umri wa miaka 43, hakutoa sababu zozote za kujiuzulu kwake.

Hata hivyo, duru zinasema kuwa kocha huyo ameamua kuondoka kwa sababu hajalipwa mshahara wake kwa muda mrefu lakini pia hafurahishwi namna maslahi ya wachezaji yanavyoshughulikiwa.

Alijiunga na mabingwa hao 15 wa ligi kuu nchini Kenya mwaka uliopita baada ya kuondoka kwa Frank Nuttall raia Scotland.

Ze Maria, ameushukuru uongozi wa Gor Mahia kwa kumwamini na kumpa nafasi ya kuifunza klabu hiyo kubwa nchini Kenya.

Aliisadia Gor Mahia kumaliza nafasi ya pili katika ligi kuu ya soka nchini humo msimu uliopita.

Mara ya mwisho kuonekana na klabu hiyo, ilikuwa ni wakati wa fainali ya kuwania taji la Sportpesa kati ya AFC Leopards jijini Dar es salaam nchini Tanzania mwishoni mwa wiki iliyopita, na kuisaidia kunyakua taji hilo.

Uongozi wa klabu hiyo umesema nafasi ya Ze Maria sasa itachukuliwa na kocha msaidizi Zedekiah ‘Zico’ Otieno ambaye pia aliwahi kuichezea klabu hiyo.

More in East Africa