Connect with us

 

Rais na mmiliki wa klabu ya soka ya TP Mazembe nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Moise Katumbi Chapwe, amehukumiwa jela miaka mitatu.

Hukumu hiyo imetolewa na Mahakama mjini Lubumbashi baada ya kumpata na kosa la kutumia mbinu za kitapeli kununua nyumba ya kifahari kutoka raia wa Ugiriki mjini Lubumbashi.

Hii inakuja baada ya tajiri huyo mwenye umri wa maiak 51, kuondoka nchini DRC kwenda nchini Uingereza kutibiwa mwezi Mei baada ya serikali kumfungulia mashtaka ya kutishia usalama wa nchi kwa madai kuwa alikuwa amewaajiri mamluki kutoka Marekani kumlinda.

Masaibu ya Katumbi yamekuja baada ya kutangaza miezi kadhaa iliyopita kuwania urais kupitia vyama vya upinzani na kupambana na rais wa sasa Jospeh Kabila kama atawania.

Katumbi ambaye ni maarufu nchini mwake na aliyewahi kuwa Gavana wa jimbo la Katanga, amekuwa akisema analengwa kisiasa baada ya kutangaza kuwania urais na kukihama chama tawala.

Klabu yake kwa sasa inashiriki katika michuano ya Shirikisho barani Afrika hatua ya makundi na mwishoni mwa juma lililopita, ilishinda Medeama FC ya Ghana mabao 3 kwa 1 mjini Lubumbashi.

More in