Connect with us

Wakati kombe la dunia, likianza nchini Urusi, tuangazie baadhi ya Manahodha wanaonekana kuvutia hisia za mashabiki wa soka pamoja na kuangaliwa sana.

Essam El Hadary (Misri)

Atakuwa nahodha na kipa wenye umri mkubwa zaidi kuwahi kushiriki katika historia ya kombe la dunia, akiwa na umri wa miaka 45.

El Hadary, anatarajiwa kuvunja rekodi ya aliyekuwa kipa wa Colombia Faryd Mondragon ambaye aliichezea nchi yake akiwa na umri wa miaka 43 mwaka 2014 nchini Brazil.

Amekuwa akiichezea timu ya taifa tangu mwaka 1996, na kuwa langoni katika mechi zaidi ya 150.

Harry Kane (Uingereza)

Kane ana umri wa miaka 24, nahodha mwenye umri mdogo sana katika michuano hii.

Uwezo wake wa kuongoza na kuwashawishi wachezaji wenzake, kulimpa nafasi hiyo, ambayo imewahi kushikiliwa na wachezaji wengine wa zamani kama Wayne Rooney, John Terry, David Beckham na Gary Lineker.

Kocha Gareth Southgate anaamini kuwa mshambuliaji huyu wa Tottenham Hotspur ambaye amefunga mabao zaidi ya 1000 kwa misimu minne iliyopita, atasaidia wachezaji wenzake kufanya vizuri.

Neymar (Brazil)

Ni mmoja wa wachezaji wakubwa wa soka duniani.

Neymar mwenye umri wa miaka 26, amepewa kibarua kizito cha kuisaidia nchi yake kunyakua kombe la dunia kwa mara ya sita.

Wachambuzi wa soka na raia wa Brazil wanasubiri kuona namna Neymar atakavyokiongoza kikosi cha Seleção kama kinachofahamika kwa jina lingine.

Aron Gunnarsson (Iceland)

Ataongoza kikosi cha nchi yake inayoshiriki katika michuano ya kombe la dunia kwa mara ya kwanza.

Aron mwenye umri wa miaka 29, amekuwa akiichezea nchi yake tangu mwaka 2008 na amekuwa nahodha tangu mwaka 2012.

Mwaka 2016, aliisaidia nchi yake kufuzu katika michuano ya bara Ulaya kwa mara ya kwanza.

Radamel Falcao (Colombia)

Amerejea katika kikosi cha timu ya taifa, baada ya jeraha kumkosesha kombe la dunia mwaka 2014 nchini Brazil.

Lengo la Falcao mwenye umri wa miaka 32 ni kuisaidia nchi yake kufika fainali ya taji hilo, baada ya mwaka 2014 kufanikiwa kuingia katika hatua ya robo fainali.

Mshambuliaji huyu anatumaini ataisaidia nchi yake kuingia katika vitabu vya historia.

 

More in