Connect with us

Yanga yapata alama tatu muhimu Morogoro

Yanga yapata alama tatu muhimu Morogoro

Mabingwa wa ligi kuu ya soka Tanzania bara Yanga FC wamepata alama tatu muhimu na kuendelea kuongoza ligi baada ya kuifunga Mtibwa Sugar mabao 2 kwa 0.

Mchuano huo ulichezwa siku ya Jumatano katika uwanja wa CCM mjini Morogoro na kuhudhuriwa na mamia ya mashabiki wa Yanga waliosafiri kutoka jijini Dar es salaam.

Mtibwa Sugar waliokuwa nyumbani walionekana kuibana Yanga FC katika kipindi cha kwanza cha mchezo huo na hadi muda wa mapumziko, hakuna aliyekuwa amepata bao.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku timu zote mbili zikionekana kutumia nguvu lakini makosa ya mabeki ya Mtibwa Sugar yalimpa nafasi mshambuliaji wa Yanga Malimi Busungu kuandikisha bao la kwanza.

Donald Ngoma naye aliihakikishia ushindi klabu yake kwa kuipa bao la pili muda mfupi kabla ya mchuano huo kumalizika.

Yanga wanaendelea kuongoza ligi kwa alama 15 baada ya michuano mitano.

Mchuano mwingine uliochezwa siku ya Jumatano ni kati ya wekundu wa Msimbazi Simba FC ambao walipata ushindi wa bao 1 kwa 0 dhidi ya Stand United katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Azam FC nao wakiwa katika uwanja wao wa nyumbani wa Azam Complex viungani mwa jijini la Dar es salaam katika mitaa ya Chamazi, waliifunga Coastal Union mabao 2 kwa 0.

Siku ya Alhamisi Toto Africans watachuana na Mbeya FC.

Bedjos Solutions Bondo

Must See

More in